Thursday, 26 March 2015

DOMINIKA YA MATAWI, MWAKA B. MARCH 29, 2015

Masomo ya Kumbukumbu ya Kuingia Bwana Yerusalemu kwa Shangwe
Mk 11:1-10 au Yn 12:12-16
Somo I. Isa. 50:4-7, Somo la II. Flp 2:6-11, Inj. Mk 14:1-15,47

Kanisa leo linaadhimisha dominika ya matawi ya mateso. Ni dominika ya matawi kwasababu tunakumbuka  kuingia Bwana Yerusalemu kwa shangwe ambako alishangiliwa na watu kwa kutikisa matawi ya mitende akiwa amepanda punda. Tunafanya kumbukumbu hiyo kwa kubariki matawi na kuingia kanisani kwa maandamano tukiongozwa na padre anayemwakilisha Kristu na kutikisa matawi yetu tukiimba hosanna mwana wa daudi. Dominika hii huitwa ya mateso pia kwa sababu inatuingiza kwenye wiki kuu ambamo tunaadhimisha mateso kifo na kuzikwa kwa Bwana wetu Yesu Kristu. Kumbukumbu ya kuingia kwa Bwana Yerusalemu kwa shangwe ikiishia tu kuwa ishara ya nje haitakuwa na umuhimu kwetu kwa hiyo ni vema basi tukatakafakari juu ya maana ya ishara hiyo ili dhimisho la leo lizae matunda ndani yetu.

Tukio la Bwana kuingia Yerusalem kwa shangwe laonesha ujasiri wa Yesu wa kuyakabili mateso yake mwenyewe kwa ajili ya ukombozi wetu. Yesu anaingia Yerusalem wakati saa yake ikiwa imefika yaani muda muafaka wa kukamatwa, kuteswa na  kuuawa kwa ajili ya ukombozi wetu. Yesu akijua haya yote na ya kwamba yatatokea Yerusalem, walipo wakuu wa mahukani na mafarisayo waliowaka hasira na chuki dhidi yake; wakitafuta nafasi ya kumkamata kwa udi na uvumba, anaingia Yerusalemu kwa uwazi akiwa amepanda punda akijionesha mbele ya umma wa watu bila kuogopa watesi wake. nay a kwambahaya yote yatatokea Yerusalem. Katika hali ya kawaida ya mwanadamu Yesu angeingia Yesrusalem kwa siri na kujificha ili watesi wake wasimuone au pengine wapate shida kidogo katikaa kumtafuta. Lakini yesu anawarahisishia kazi kwa kuingia kwa uwazi. Anatufundisha ujasiri katika kupokea mateso ambayo hayaepukiki katika maisha yetu kwa ajili ya kutimiza mapenzi ya Mungu

Kumbukumbu ya kuingia Yerusalemu kwa shangwe inatufundisha kuwa daima tumtafute Yesu kwa ajili ya wongofu ili tuwe tayari kumfuata katika hali zote za raha na taabu. Tusimfuate na kumkimbilia Yesu   kwa sababu ya kuvutwa na   uwezo wake wa kufanya miujiza au mambo yasiyokuwa ya kawaida, umahiri wake wa kuhubiri  au kwa ajili ya kutimiza malengo ya ubinafsi wetu. Kati ya watu waliokuwa wanamshangilia Yesu walikuwepo wengi waliomfuata kwa sababu walimuona akitenda miujiza mingi na hasa walivutwa na muujiza kwa kumfufua Lazaro kule Betania. Kwa ujumla wake pia wayahudi wengi walimshangilia Yesu wakidhani kuwa yeye ni masia wa kisiasa anakuja kuuupindua utawala wa Kirumi kwa mtutu ili awarudishie utawala wao. Hawakumshangilia Yesu kwa sababu ni Masiya anayekuja kuwatoa kwenye utawala wa dhambi. Kwa sababu ya malengo hayo potofu ndio maana watu wote waliomshangilia ndio waligeuka kuwa maadui wake pale msalabani

Tunaalikwa leo tuwe tayari kufungua mioyo yetu ili tusikie sauti ya Mungu na tujifunze mapenzi yake kwetu. Yesu daima amekuwa akiwafundisha watu ili waelewe kuwa yeye ni nani hasa na amekuja duniani kwa ajili ya kazi gani . Lakini kutokana na ugumu wa mioyo ya watu na hasa kwa sababu ya  ubinafsi hawakuwa tayari kusikia. Daima walibaki na mtazamo wao wa masia wa kisiasa. Kabla ya kuingia kwenye saa yake Yesu anafanya jitihada ya mwisho ya kuwafungua macho Wayahudi ili waelewe aina ya masiya anayewajia  kwa kufanya ishara ya nje,  mbinu ilizotumiwa na  manabii waliomtangulia  ili kuwafanya Wayahudi  walelewe ujumbe wa Mungu baada ya kushindwa kwa maneno, unaweza  kurejea (1Fal 11:30-2). Kwa kawaida Huko Palestina punda ni mnyama mwenye hadhi kubwa sana. Ni mnyama anayetumiwa na mfalme wakati wa amani. Kukiwa na vita mfalme hutumia farasi. Yesu anaamua kuingia Yerusalemu kwa shangwe akiwa amepanda punda ili awafundishe kuwa yeye ni mfalme na masia lakini ni mfalme wa amani na upendo na wala si mfalme wa vita. Pamoja na kufanya hayo yote Wayahudi walishindwa kumuelewa kwa sababu mioyo yao ilifungwa na ubinafsi wao. Nasi tukiruhusu ubinafsi wetu ututawale hatutatoa nafasi ya kusikiliza sauti ya Mungu inayoutuelekeza kutimiza mapenzi yake.

Kristu anapoamua kupanda punda kama ishara ya mfalme wa amani  anatufundisha kuwa silaha bora ya kupambana na adui ni upendo, huruma na amani. Wayahudi walikuwa na adui ambaye ni utawala wa Kirumi uliwofanya kuwa koloni lao. Walimsubiria mkombozi atakayekuja kumshinda adui huyu na kumtoa  kwa upanga ili awarudishie utawala wao, lakini kwa kupanda punda Yesu anawaambia kuwa yeye ni Mkombozi anayekuja kupambana na adui kwa kumpa upendo na uhuruma ili  adui huyu aguswe  dhamiri yake na abadilike kuwa mtu mwema.

Wayahudi waliimba hosanna mwana wa Daudi wakimaanisha utuokoe kutoka lugha ya kiebrania. Kama ambavyo tumeona hapo awali, wokovu walioutarajia wayahudi kutoka kwa Yesu ni wokovu wa kisiasa yaani Yesu awaongoze katika vita ya kuwaondosha Warumi katika nchi yao na kuwapatia uhuru. Sisi tunapoimba  leo hosanna mwana wa Daudi  tunamuita  Yesu atuokoe kwanza kiroho yaani atuongoze katika vita ya kumng’oa Shetani katika roho zetu na kutupatia uhuru wetu wa roho ili tuwe na amani na furaha.  Lakini zaidi ya hapo tukisha okoka ndani yetu , Yesu atuokoe katika mifumo dhalimu ya kisiasa, kiuchumi na kijamii inayowafanya watu wateseke kwa kukosa chakula, malazi, afya bora, elimu na haki nyingine nyingi za binadamu


Tumuombe Mungu ili dominika ya leo ituingize vyema katika tafakari ya mateso na kifo cha Bwana wetu Yesu Kristu tusije tukafanana  na wale wa wayahudi ambao walimshangilia lakini muda mfupi baadae walimgeuka. Tufanane na mama bikira Maria na yule mwanafunzi, waliolewa maana ya Kristu kuteseka na wakakubali kuteseka pamoja naye ili wapate wokovu. 

Thursday, 19 March 2015

DOMINIKA YA TANO YA KWARESIMA, MWAKA B. March 22, 2015

Somo I:  Yer. 31:31-34, Somo II: Ebr. 5:7-9, Injili : Yn. 12:20-33

Tumebakiza wiki moja kabla ya kuadhimisha mateso na kifo cha Kristu. Katika dominika ya leo kanisa linaanza kutuingiza katika tafakari ya mateso ya Kristu. Neno la Mungu leo linatufunulia ukweli kuhusu thamani ya mateso ya Kristu ambaye aliteseka kama wanadamu wengine. Ili kuweza kuona thamani ya mateso katika maisha inategemea namna tunavyoyapokea. Kristu aliyapokea mateso kwa imani na hivyo Baba yake wa Mbinguni akamuonesha thamani hiyo na kumpa uhakika wa utukufu baada ya mateso. Baada ya kuelewa thamani hiyo Kristo alitii sauti ya Mungu katika kuyakabili mateso

Katika somo la kwanza nabii Jeremia anawapa Waisraeli habari njema ya Mungu kufanya agano jipya nao. Katika agano hili jipya Mungu anasisitiza juu ya uhusiano wake na mwanadamu unaodai kujitoa bila kujibakiza ndani ya moyo wa mtu. Anaposema kuwa ataiandika sheria yake ndani ya moyo wa mtu anamanisha kuwa anataka watu wampende Mungu si kwa matendo ya nje tu bali kwa moyo na akili zao zote. Watu wote watamjua Mungu ndani ya mioyo yao kwa sababu watakuwa wameondolewa giza la dhambi ya asili kwa agano hili jipya. Waisraeli walivunja agano la wanza kwasababu walisisitiza zaidi juu ya uhusiano wao na Mungu kwa matendo ya nje kuliko kujitoa nafsi. Kujitoa nafsi kwa ajili ya Mungu kunahitaji kutoa sadaka kubwa. Hakuna sadaka kubwa isiyokuwa na maumivu au mateso. Tunapokosa ujasiri wa kuyakabili mateso na  maumivu hayo hautewezi kuwa waaminifu kwa agano.

Katika somo la pili mwandishi kwa Waebrania anamuonesha Kristu Kuhani mkuu aliyetesekea pamoja nasi ili atufundishe namna ya kuyakabili mateso. Kwa sababu ya uchungu mkubwa anaoupata Kristu kutokana na mateso sala yake kwa Mungu ni ya kilio cha sauti na kumwaga machozi kama ilivyo kwa mwanadamu mwingine yeyote anapokuwa katika mateso makali. Kristu anatufundisha kupokea mateso kwa imani ili tuweze kujifunza mapenzi ya Mungu kwetu katika mateso yake. Kristu alijifunza kuwa mateso yake ni kwa ajli ya ukombozi wetu na baada ya kutambua hilo anakubali kutii mapezni ya Mungu.  Kwa sababu ya kupokea mateso kwa imani mateso yanamfanya Kristu awe mkamilifu katika kazi yake , hivyo nafsi tukiyapokea mateso kwa imani  tunakuwa wakamilifu katika kumtumikia Mungu.

Katika somo la injili Kristu anatufundisha kuwa kukubali na kupokea mateso yanayotokana na kujikana nafsi zetu, kutolea sadaka yale tunayoyapenda sana, kujikatalia haki zetu ikibidi haki ya kuishi kwa ajili ya kumtumikia Mungu na watu tutatoa mazao mengi na tutazisalimisha nafsi zetu katika uzima wa milele. Tutatoa mazao kama vile upendo, unyenyekevu , uvumilivu, msamaha na utu wema. Kuamua kutii mapenzi ya Mungu katika mateso makali kuna ugumu mkubwa, kuna hofu nyingi  na kunahitaji sadaka kubwa. Hivyo kutii kwa kweli ni kuamuna kusonga mbele katika hofu nyingi na kushinda na hapa ndipo penye fadhila. Kristu alikabiliana na ugumu na hofu nyingi katika kuamua kutiii mapenzi ya Mungu katika mateso yake. Alifika mahali alimuomba Baba amuepushe na saa ya mateso lakini alikabiliana na hofu na ugumu wote na akaweza kutii. Tukiwa watu wa  sala daima Mungu hatuachi peke yetu katika kuyakabili mateso. Atakuwepo kwa ajili ya kututia moyo, atatuonesha mapenzi yake na namna ya kutii sauti yake. Katika injili Yesu anapokuwa na mahangaiko na hofu nyingi kuhusu mateso atakayoyapata sauti inatoka mbinguni na kumhakikishia kuwa mwisho wa mateso hayo ni utukufu.

Mwanadamu anapitia mateso mbalimbali katika maisha yake. Yapo mateso yanayotokana na dhambi zake mwenyewe, mateso haya si ya kuyakimbilia tunapaswa kufanya juhudi ya kuyaepuka. Kristu amekuja kutuondolea mateso haya kwa kifo chake msalabani na tukitaka kuendelea kuyaepuka ametuachia sakramenti zake na hasa ya ekaristi na kitubio. Yapo mateso ambayo hatuwezi kuyaepuka kwa sababu ya udhaifu wa miili yetu, kwa mfano, mateso yatokanayo na magonjwa. Haya ni mateso ambayo hata Kristu mwenyewe hakuyaondoa katika ulimwengu huu. Badala yake ametufundisha namna ya kuyakabili kwa imani ili tuweze kutambua mapenzi yake kwetu. Mateso haya tukiyapokea kwa imani na matumaini yanatusaidia katika malipizi ya dhambi zetu na za ulimwengu. Yapo mateso mengine ambayo hayaepukiki ikiwa tunataka kuwa wakimilifu kiroho na hata kimwili, mateso haya yanatokana na uamuzi wetu wa kujikatalia nafsi zetu, mambo tunayoyapenda kwa ajili ya Mungu na jirani. Unapojikatalia chakula katika kipindi hiki cha kwaresima unapata maumivu ya njaa lakini lengo lako ni kujitawala katika chakula ili upate nafasi ya kujibandua katika vitu vinavyopita na kukuza uhusiano wako na Kristu


Tunapoadhimisa dominika hii ya tano tumuombe Mungu atujalie kupokea mateso kwa moyo wa imani na matumaini ili tustahilishwe wokovu kwa mateso hayo.