Thursday, 19 March 2015

DOMINIKA YA TANO YA KWARESIMA, MWAKA B. March 22, 2015

Somo I:  Yer. 31:31-34, Somo II: Ebr. 5:7-9, Injili : Yn. 12:20-33

Tumebakiza wiki moja kabla ya kuadhimisha mateso na kifo cha Kristu. Katika dominika ya leo kanisa linaanza kutuingiza katika tafakari ya mateso ya Kristu. Neno la Mungu leo linatufunulia ukweli kuhusu thamani ya mateso ya Kristu ambaye aliteseka kama wanadamu wengine. Ili kuweza kuona thamani ya mateso katika maisha inategemea namna tunavyoyapokea. Kristu aliyapokea mateso kwa imani na hivyo Baba yake wa Mbinguni akamuonesha thamani hiyo na kumpa uhakika wa utukufu baada ya mateso. Baada ya kuelewa thamani hiyo Kristo alitii sauti ya Mungu katika kuyakabili mateso

Katika somo la kwanza nabii Jeremia anawapa Waisraeli habari njema ya Mungu kufanya agano jipya nao. Katika agano hili jipya Mungu anasisitiza juu ya uhusiano wake na mwanadamu unaodai kujitoa bila kujibakiza ndani ya moyo wa mtu. Anaposema kuwa ataiandika sheria yake ndani ya moyo wa mtu anamanisha kuwa anataka watu wampende Mungu si kwa matendo ya nje tu bali kwa moyo na akili zao zote. Watu wote watamjua Mungu ndani ya mioyo yao kwa sababu watakuwa wameondolewa giza la dhambi ya asili kwa agano hili jipya. Waisraeli walivunja agano la wanza kwasababu walisisitiza zaidi juu ya uhusiano wao na Mungu kwa matendo ya nje kuliko kujitoa nafsi. Kujitoa nafsi kwa ajili ya Mungu kunahitaji kutoa sadaka kubwa. Hakuna sadaka kubwa isiyokuwa na maumivu au mateso. Tunapokosa ujasiri wa kuyakabili mateso na  maumivu hayo hautewezi kuwa waaminifu kwa agano.

Katika somo la pili mwandishi kwa Waebrania anamuonesha Kristu Kuhani mkuu aliyetesekea pamoja nasi ili atufundishe namna ya kuyakabili mateso. Kwa sababu ya uchungu mkubwa anaoupata Kristu kutokana na mateso sala yake kwa Mungu ni ya kilio cha sauti na kumwaga machozi kama ilivyo kwa mwanadamu mwingine yeyote anapokuwa katika mateso makali. Kristu anatufundisha kupokea mateso kwa imani ili tuweze kujifunza mapenzi ya Mungu kwetu katika mateso yake. Kristu alijifunza kuwa mateso yake ni kwa ajli ya ukombozi wetu na baada ya kutambua hilo anakubali kutii mapezni ya Mungu.  Kwa sababu ya kupokea mateso kwa imani mateso yanamfanya Kristu awe mkamilifu katika kazi yake , hivyo nafsi tukiyapokea mateso kwa imani  tunakuwa wakamilifu katika kumtumikia Mungu.

Katika somo la injili Kristu anatufundisha kuwa kukubali na kupokea mateso yanayotokana na kujikana nafsi zetu, kutolea sadaka yale tunayoyapenda sana, kujikatalia haki zetu ikibidi haki ya kuishi kwa ajili ya kumtumikia Mungu na watu tutatoa mazao mengi na tutazisalimisha nafsi zetu katika uzima wa milele. Tutatoa mazao kama vile upendo, unyenyekevu , uvumilivu, msamaha na utu wema. Kuamua kutii mapenzi ya Mungu katika mateso makali kuna ugumu mkubwa, kuna hofu nyingi  na kunahitaji sadaka kubwa. Hivyo kutii kwa kweli ni kuamuna kusonga mbele katika hofu nyingi na kushinda na hapa ndipo penye fadhila. Kristu alikabiliana na ugumu na hofu nyingi katika kuamua kutiii mapenzi ya Mungu katika mateso yake. Alifika mahali alimuomba Baba amuepushe na saa ya mateso lakini alikabiliana na hofu na ugumu wote na akaweza kutii. Tukiwa watu wa  sala daima Mungu hatuachi peke yetu katika kuyakabili mateso. Atakuwepo kwa ajili ya kututia moyo, atatuonesha mapenzi yake na namna ya kutii sauti yake. Katika injili Yesu anapokuwa na mahangaiko na hofu nyingi kuhusu mateso atakayoyapata sauti inatoka mbinguni na kumhakikishia kuwa mwisho wa mateso hayo ni utukufu.

Mwanadamu anapitia mateso mbalimbali katika maisha yake. Yapo mateso yanayotokana na dhambi zake mwenyewe, mateso haya si ya kuyakimbilia tunapaswa kufanya juhudi ya kuyaepuka. Kristu amekuja kutuondolea mateso haya kwa kifo chake msalabani na tukitaka kuendelea kuyaepuka ametuachia sakramenti zake na hasa ya ekaristi na kitubio. Yapo mateso ambayo hatuwezi kuyaepuka kwa sababu ya udhaifu wa miili yetu, kwa mfano, mateso yatokanayo na magonjwa. Haya ni mateso ambayo hata Kristu mwenyewe hakuyaondoa katika ulimwengu huu. Badala yake ametufundisha namna ya kuyakabili kwa imani ili tuweze kutambua mapenzi yake kwetu. Mateso haya tukiyapokea kwa imani na matumaini yanatusaidia katika malipizi ya dhambi zetu na za ulimwengu. Yapo mateso mengine ambayo hayaepukiki ikiwa tunataka kuwa wakimilifu kiroho na hata kimwili, mateso haya yanatokana na uamuzi wetu wa kujikatalia nafsi zetu, mambo tunayoyapenda kwa ajili ya Mungu na jirani. Unapojikatalia chakula katika kipindi hiki cha kwaresima unapata maumivu ya njaa lakini lengo lako ni kujitawala katika chakula ili upate nafasi ya kujibandua katika vitu vinavyopita na kukuza uhusiano wako na Kristu


Tunapoadhimisa dominika hii ya tano tumuombe Mungu atujalie kupokea mateso kwa moyo wa imani na matumaini ili tustahilishwe wokovu kwa mateso hayo.

No comments:

Post a Comment