Thursday, 26 March 2015

DOMINIKA YA MATAWI, MWAKA B. MARCH 29, 2015

Masomo ya Kumbukumbu ya Kuingia Bwana Yerusalemu kwa Shangwe
Mk 11:1-10 au Yn 12:12-16
Somo I. Isa. 50:4-7, Somo la II. Flp 2:6-11, Inj. Mk 14:1-15,47

Kanisa leo linaadhimisha dominika ya matawi ya mateso. Ni dominika ya matawi kwasababu tunakumbuka  kuingia Bwana Yerusalemu kwa shangwe ambako alishangiliwa na watu kwa kutikisa matawi ya mitende akiwa amepanda punda. Tunafanya kumbukumbu hiyo kwa kubariki matawi na kuingia kanisani kwa maandamano tukiongozwa na padre anayemwakilisha Kristu na kutikisa matawi yetu tukiimba hosanna mwana wa daudi. Dominika hii huitwa ya mateso pia kwa sababu inatuingiza kwenye wiki kuu ambamo tunaadhimisha mateso kifo na kuzikwa kwa Bwana wetu Yesu Kristu. Kumbukumbu ya kuingia kwa Bwana Yerusalemu kwa shangwe ikiishia tu kuwa ishara ya nje haitakuwa na umuhimu kwetu kwa hiyo ni vema basi tukatakafakari juu ya maana ya ishara hiyo ili dhimisho la leo lizae matunda ndani yetu.

Tukio la Bwana kuingia Yerusalem kwa shangwe laonesha ujasiri wa Yesu wa kuyakabili mateso yake mwenyewe kwa ajili ya ukombozi wetu. Yesu anaingia Yerusalem wakati saa yake ikiwa imefika yaani muda muafaka wa kukamatwa, kuteswa na  kuuawa kwa ajili ya ukombozi wetu. Yesu akijua haya yote na ya kwamba yatatokea Yerusalem, walipo wakuu wa mahukani na mafarisayo waliowaka hasira na chuki dhidi yake; wakitafuta nafasi ya kumkamata kwa udi na uvumba, anaingia Yerusalemu kwa uwazi akiwa amepanda punda akijionesha mbele ya umma wa watu bila kuogopa watesi wake. nay a kwambahaya yote yatatokea Yerusalem. Katika hali ya kawaida ya mwanadamu Yesu angeingia Yesrusalem kwa siri na kujificha ili watesi wake wasimuone au pengine wapate shida kidogo katikaa kumtafuta. Lakini yesu anawarahisishia kazi kwa kuingia kwa uwazi. Anatufundisha ujasiri katika kupokea mateso ambayo hayaepukiki katika maisha yetu kwa ajili ya kutimiza mapenzi ya Mungu

Kumbukumbu ya kuingia Yerusalemu kwa shangwe inatufundisha kuwa daima tumtafute Yesu kwa ajili ya wongofu ili tuwe tayari kumfuata katika hali zote za raha na taabu. Tusimfuate na kumkimbilia Yesu   kwa sababu ya kuvutwa na   uwezo wake wa kufanya miujiza au mambo yasiyokuwa ya kawaida, umahiri wake wa kuhubiri  au kwa ajili ya kutimiza malengo ya ubinafsi wetu. Kati ya watu waliokuwa wanamshangilia Yesu walikuwepo wengi waliomfuata kwa sababu walimuona akitenda miujiza mingi na hasa walivutwa na muujiza kwa kumfufua Lazaro kule Betania. Kwa ujumla wake pia wayahudi wengi walimshangilia Yesu wakidhani kuwa yeye ni masia wa kisiasa anakuja kuuupindua utawala wa Kirumi kwa mtutu ili awarudishie utawala wao. Hawakumshangilia Yesu kwa sababu ni Masiya anayekuja kuwatoa kwenye utawala wa dhambi. Kwa sababu ya malengo hayo potofu ndio maana watu wote waliomshangilia ndio waligeuka kuwa maadui wake pale msalabani

Tunaalikwa leo tuwe tayari kufungua mioyo yetu ili tusikie sauti ya Mungu na tujifunze mapenzi yake kwetu. Yesu daima amekuwa akiwafundisha watu ili waelewe kuwa yeye ni nani hasa na amekuja duniani kwa ajili ya kazi gani . Lakini kutokana na ugumu wa mioyo ya watu na hasa kwa sababu ya  ubinafsi hawakuwa tayari kusikia. Daima walibaki na mtazamo wao wa masia wa kisiasa. Kabla ya kuingia kwenye saa yake Yesu anafanya jitihada ya mwisho ya kuwafungua macho Wayahudi ili waelewe aina ya masiya anayewajia  kwa kufanya ishara ya nje,  mbinu ilizotumiwa na  manabii waliomtangulia  ili kuwafanya Wayahudi  walelewe ujumbe wa Mungu baada ya kushindwa kwa maneno, unaweza  kurejea (1Fal 11:30-2). Kwa kawaida Huko Palestina punda ni mnyama mwenye hadhi kubwa sana. Ni mnyama anayetumiwa na mfalme wakati wa amani. Kukiwa na vita mfalme hutumia farasi. Yesu anaamua kuingia Yerusalemu kwa shangwe akiwa amepanda punda ili awafundishe kuwa yeye ni mfalme na masia lakini ni mfalme wa amani na upendo na wala si mfalme wa vita. Pamoja na kufanya hayo yote Wayahudi walishindwa kumuelewa kwa sababu mioyo yao ilifungwa na ubinafsi wao. Nasi tukiruhusu ubinafsi wetu ututawale hatutatoa nafasi ya kusikiliza sauti ya Mungu inayoutuelekeza kutimiza mapenzi yake.

Kristu anapoamua kupanda punda kama ishara ya mfalme wa amani  anatufundisha kuwa silaha bora ya kupambana na adui ni upendo, huruma na amani. Wayahudi walikuwa na adui ambaye ni utawala wa Kirumi uliwofanya kuwa koloni lao. Walimsubiria mkombozi atakayekuja kumshinda adui huyu na kumtoa  kwa upanga ili awarudishie utawala wao, lakini kwa kupanda punda Yesu anawaambia kuwa yeye ni Mkombozi anayekuja kupambana na adui kwa kumpa upendo na uhuruma ili  adui huyu aguswe  dhamiri yake na abadilike kuwa mtu mwema.

Wayahudi waliimba hosanna mwana wa Daudi wakimaanisha utuokoe kutoka lugha ya kiebrania. Kama ambavyo tumeona hapo awali, wokovu walioutarajia wayahudi kutoka kwa Yesu ni wokovu wa kisiasa yaani Yesu awaongoze katika vita ya kuwaondosha Warumi katika nchi yao na kuwapatia uhuru. Sisi tunapoimba  leo hosanna mwana wa Daudi  tunamuita  Yesu atuokoe kwanza kiroho yaani atuongoze katika vita ya kumng’oa Shetani katika roho zetu na kutupatia uhuru wetu wa roho ili tuwe na amani na furaha.  Lakini zaidi ya hapo tukisha okoka ndani yetu , Yesu atuokoe katika mifumo dhalimu ya kisiasa, kiuchumi na kijamii inayowafanya watu wateseke kwa kukosa chakula, malazi, afya bora, elimu na haki nyingine nyingi za binadamu


Tumuombe Mungu ili dominika ya leo ituingize vyema katika tafakari ya mateso na kifo cha Bwana wetu Yesu Kristu tusije tukafanana  na wale wa wayahudi ambao walimshangilia lakini muda mfupi baadae walimgeuka. Tufanane na mama bikira Maria na yule mwanafunzi, waliolewa maana ya Kristu kuteseka na wakakubali kuteseka pamoja naye ili wapate wokovu. 

No comments:

Post a Comment