Friday, 22 May 2015

DOMINIKA YA PENTEKOSTE, MWAKA B. MAY 24, 2015

I.                    Mdo 2:1-11    II. 1 Kor 12:3b-7, 12-13  Inj. Yn 20:19-23
Siku ya hamsini ya kipindi kitakatifu cha Pasaka inahitimishwa na Dominika ya Pentekoste, kanisa linapokumbuka kazi ya Roho Mtakatifu kwa Mitume, mwanzo wa Kanisa na mwanzo wa utume wake kwa lugha, watu na mataifa yote. Roho mtakatifu analitakasa kanisa, analifariji katika mahangaiko yake ya hapa duniani na pia analiwezesha katika utume wake kupitia vipaji, karama na huduma mbalimbali anazozimimina kwa wanakanisa kadiri apendavyo

Katika injili leo Yohane anatupatia simulizi la Yesu mfufuka akiwatokea mitume katika chumba na anapowatokea anawaambia mambo kadhaa ambayo kwa kweli yanagusa pamoja na mambo mengine  utume wetu kama wana kanisa

Tunajifunza kuwa Kristu anahitaji Kanisa katika kuendeleza kazi yake ya ukombozi aliyoianzisha. Baada ya kupaa kwake mbinguni mitume wanapaswa kuwaongoza wanakanisa kwenda ulimwenguni pote na kwa kila kizazi kushuhudia ufufuko wa Kristu ili ulimwengu mzima upate wokovu. Twajua kuwa Kristu ndiye kichwa yaani Kiongozi wa Kanisa lakini anahitaji miguu, mdomo na mikono ya kupeleka ujumbe wake kwa watu wote akiwa ameketi kuume kwa Baba. Kanisa ndio miguu, mikono na mdomo wake. Kristu anategemea kanisa lenye wanadamu wasio wakamilifu wanaopambana kuufikia wokovu wao wenyewe kwanza halafu watu wengine. Kwa hiyo ni wazi kwamba kushuhudia wanakanisa wakianguka katika udhaifu  isiwe kigezo cha kukata tamaa na kulikimbia kanisa kwa sababu Kristu mwenyewe amechagua Kanisa dhaifu lifanye kazi yake.

Katika kufanya kazi ya utume Kanisa linamuhitaji sana Kristu. kwa sababu kanisa linafanya kazi ya utume hivyo lazima kuwepo na yule aliyelituma, ujumbe wa kupeleka, nguvu na mamlaka ya kupelekea ujumbe huo. Kristu ndiye anayelituma Kanisa, na analipa ujumbe wa wokovu kwa watu wote na zaidi ya hayo analipatia nguvu na mamlaka ya kupeleka ujumbe huo kupitia Roho Mtakatifu tunayempokea leo katika sherehe ya Pentekoste. Katika udhaifu wake kanisa linahitaji kujishikamanisha na Kristu daima ili liweze kufanikiwa maana Kristu mwenyewe anatuambia bila yeye hatuwezi chochote.

Kama Baba alivyomtuma Mwana ulimwenguni ndivyo Kristu anavyolituma Kanisa lake. Utume wa Kristu uliwezekana na ulifanikiwa kwa sababu tu Kristu alikuwa mtii kwa yule aliyemtuma na pia alimpenda sana. Kanisa linamwakilisha Kristu duniani hivyo daima linapaswa kuwa mtii kwake ili lisije kupeleka ujumbe wake badala ya ujumbe wa Kristu. Upendo ndio msingi wa utume wetu, yatupasa kuwa tayari kutolea maisha yetu kwa ajili ya yule aliyetutuma

 Kristu anatualika tupeleke ujumbe wa msamaha wake kwa wadhambi wanaotubu. Anapowaeleza mitume wake juu ya mamlaka ya kufunga na kufungua anawatuma waende ulimwenguni kote na kuwaeleza watu kuwa Kristu alikuja duniani kuwasamehe watu makosa yao. Atakayekuwa tayari kutubu na kuomba msamaha atasamehewa lakini yule anayekataa msamaha wake hatapokea msamaha huo.

Katika somo la pili mtume Paulo anatueleza kuwa utume wa kanisa unawezekana kwa sababu Roho Mtakatifu anagawa karama, vipaji na huduma mbalimbali kwa watu wake. Kupitia karama hizi wanakanisa wanapeleka ujumbe wa Kristu kwa watu. Karama mbalimbali zinatolewa kwa ajili ya manufaa ya Kanisa zima na wala si kwa ajili ya sifa na utukufu wa wale waliojaliwa karama hizo

Somo la kwanza ni simulizi la tukio la Pentekoste ambalo kwa kweli linaonesha kazi ya Roho Mtakatifu kwa mitume, mwanzo wa Kanisa, mwanzo wa utume wa kanisa kwa lugha, watu na mataifa yote. Ni muhimu kuelewa awali ya yote kwamba Roho Mtakatifu yupo na amekuwepo daima akifanya kazi kati ya watu hata kabla ya tukio hili ya Pentekoste. Ingawaje ni ukweli kwamba kuna kitu cha pekee kilitokea siku hiyo ya Pentekoste. Siku ya Pentekoste Roho Mtakatifu aliwavuvia mitume na kuwapa zawadi na karama ya ajabu ambayo hawakuwahi kuipata kabla. Uvuvio huu wa Roho Mtakatifu uliwafanya mitume walihubiri neno la Mungu kwa namna ambayo kwa mara ya kwanza iligusa mioyo ya watu na walielewa vizuri sana.

Wapo watu wanaosema kuwa mitume walipata uwezo wa kunena kwa lugha kama ishara ya kuvuviwa na Roho Mtakatifu. Kunena kwa lugha kunakozungumziwa na ule uwezo wa kutamka maneno ambayo hakuna mtu mwingine anayeweza kuelewa, jambo ambalo lilikuwepo hata katika kanisa la mwanzo. Watu hawa wanaenda mbali zaidi na kudai kuwa hiyo ndio ishara ya muhimu na ya pekee ya uwepo wa Roho Mtakatifu. Mtume Paulo ameeleza kwa kirefu juu ya kipawa cha kunena kwa lugha katika (1Kor 14) lakini kwa ufupi anachoeleza ni kuwa kipaji chochote anachotoa Roho Mtakatifu ni kwa ajili ya manufaa ya jumuiya, la kama mtu amepewa kipaji na hakiwasaidiii wanajumuiya katika kuabudu kwao isipokuwa yule aliyepewa basi asikitumie katikati ya wanajamii hasa katika sala. Zaidi ya hayo hatuwezi kusema kuwa kiuongo kimoja katika mwili ndio chenye umuhimu kuliko vingine kwa sababu ili mwili uitwe mwili unahitaji kuwa na viunguo vyote kamili na ndio maana wasio na viungo fulani huitwa walemavu ingawaje hawajapoteza utu wao. Haiwezekani kipaji kimoja tu ndio kikawa muhimu kuliko kingine katika mwili wa fumbo wa Kristu yaani Kanisa.


Hivyo katika pentekoste si kwamba mitume walipata hiyo karama ya kunena kwa lugha kwa sababu kila walichokiongea watu walikielewa. Kipaji cha kunena kwa lugha kadiri ya Paulo ni kwa ajili ya yule tu mwenye kipaji hicho na watu wengine hawawezi kumuelewa. 

No comments:

Post a Comment