Thursday, 14 May 2015

DOMINIKA YA SABA YA PASAKA, MWAKA B. MAY 17, 2015

Mdo 1:15-17, 20a, 20c-26,  I Yoh 4:11-16, Inj. Yn 17:11b-19

Wakristu tunao uhakika kuwa  kiongozi wetu Yesu Kristu hata baada ya kupaa kwake mbinguni anaendelea kuwa pamoja nasi kutuongoza, kutuimarisha, kutubariki katika safari yetu ya kuelekea kule aliko yeye. Kwa mara nyingine leo tunakumbushwa kuwa ukristu wetu unatudai mambo makubwa sana yanayohitaji kujitoa mhanga kwa ajili ya Kristu kiongozi wetu. Peke yetu hatuwezi ni lazima tuombe msaada wake kwa njia ya sala yeye aliyetuahidi kuwa pamoja nasi mpaka mwisho wa safari.

Katika njili Yesu kuhani mkuu analiombea kundi lake kabla ya kuteswa, kufa, kufufuka na kupaa kwake mbinguni. Katika sala ya Yesu tunaweza pamoja na mambo mengi tukatafakri mambo makubwa manne kuhusu ukristu wetu.

Mkristu safi, hodari na shujaa si yule anayejitenga na ulimwengu bali yule anayeishi ndani ya ulimwengu lakini anaushinda ulimwengu. Yesu haombi kwamba tutoke ulimwenguni bali tulindwe na yule mwovu. Mara nyingi nimesikia watu mbalimbali walio katika ndoa wanawaambia mapadre na watawa kuwa afadhali wao wamechagua maisha ya kujitenga na ulimwengu kwa kuwa watawa  au  mapadre kwani wameepukana na maouvu ya ulimwengu. Ingawaje si kweli kwamba mapadre na watawa wametoka katika ulimwengu huu lakini hoja ya watu wanaofikiri hivyo kuhusu mapadre ni kwamba mtu atakuwa mkristu mzuri kama atatoka katikati ya ulimwengu uliojaa maovu jambo ambalo si la kweli. Wapendwa maisha ya ukristu maana yake ni kwenda kinyume na ulimwengu huo huo tunaoishi. Tunapaswa kuwa mashuhuda wa Kristu, kwa mfano, katika ulimwengu unaotumia mitandao ya kijamii kubomoa maaadili kwa sisi kutumia mitandao hiyo vizuri na si kuacha kutumia. Ukristu hautuweki huru dhidi ya matatizo bali unatupa mbinu za kupambana na matatizo

Wakristu tumewekwa wakfu yaani tumetengwa kwa ajili ya kazi maalumu. Sehemu ya mwisho ya sala ya kristu katika injili ya leo yaeleza ukweli huu Kristu anapoomba tutakaswe na hiyo kweli. Tumezoea kuwa mapadre na watawa tu ndio wamewakwa wakfu lakini ukweli ni kwamba kwa ubatizo wetu sisi sote tumetengwa kwaajili ya kazi maalumu ya kumshuhudia Kristu popote ulimwenguni kwa maneno na matendo yetu. Ni kweli kwamba mapadre na watawa wamewekwa wakfu kwa namna ya pekee lakini hili halifuti ukweli kuwa kila mbatizwa amewekwa wakfu kuwa shahidi wa Kristu. Kila mkristu popote alipo anapaswa kutambua kuwa yeye ni mteuliwa wa Kristu, ametengwa kwa ajili ya kumtambulisha Kristu kwa watu kwa utakatifu wake. Unapokuwa shuleni, sehemu ya kazi, nyumbani unapaswa kutambua kuwa wewe umechaguliwa na Kristu kuwa mfano wa maisha ya utakatifu, kinyume cha hapo unakufuru kwa kutenda uovu.

Silaha ya kumshinda mwovu hapa duniani ni kwa wakristu kuwa na umoja. Ni kwa bahati mbaya sana kati ya vitu ambavyo Kristu aliliombea kanisa lake umoja wa wakristu umepata misukosuko mingi. Wakristu wanapaswa kuwa na roho moja na moyo mmoja katika Kristu. Wapo watu katika ulimwengu huu ambao wanatumia silaha ya utengano kwa wakristu ili kujinufaisha katika mambo yao. Tumeona mara kadhaa wanasiasa wanavyovuruga kanisa ili likose msimamo mmoja katika kutetea maadili mema na hivyo wapate nafasi ya kukanyaga haki za watu kwa manufaa yao binafsi.

Wakristu tuna uhakika wa ulinzi wa Kristu dhidi ya mwovu tukiwa ulimwenguni. Yesu anatulinda kwa kweli ili tusiingie katika mtego wa shetani wa kutenda dhambi. Ulinzi huu tutaupata ikiwa tutakuwa tayari kuutafuta. Mara kadhaa kumekuwa na maswali inakuwaje watu wasio na hatia wanateseka na kufa kutokana na makosa ya watu wengine ikiwa Kristu anatuombea kwa Baba ili tulindwe na huyo mwovu. Si rahisi sana kusema kwa uhakika kwa nini haya yanatokea kwa sababu mateso bado ni fumbo kwetu. Lakini sisi wakristu daima tunaalikwa kumuangalia Kristu kiongozi wetu ambaye aliishi kila kitu sawa na sisi isipokuwa hakutenda dhambi, na bado akafa kifo cha aibu msalabani. Ufufuko wake umedhihirisha kuwa mateso ya mwili kwa mkristu si kitu ikiwa ameishi akiwa anamwamini Kristu. Hivyo pale inapotokea watu wasio na hatia wanateswa  na kufa na wakati mwingine kwa sababu ya imani yao, hatupaswi kumlaani Mungu kwa kudhani kuwa Mungu hayupo au hatupendi.

Somo la kwanza latutafakarisha juu ya wajibu wetu wa Kikristu. Katika kumchagua mtu atakayekuwa mbadala wa Yuda Iskariote wakristu wakwanza  waliongozwa na neno hili kuwa anapaswa awe shahidi wa ufufuko wa Kristu. katika somo hilo tunaelezwa jinsi ambavyo kanisa letu lenye watu zaidi ya bilioni leo hii lilikuwa na watu 120 tu wakati Matiya anachaguliwa kuwa mbadala wa Yuda. Inaonesha jinsi gani wakristu wa kwanza walifanya kazi kubwa ya kushuhudia ufufuko wa Kristu kiasi cha mimi na wewe leo kuitwa wakristu na huo ndio wajibu wetu mkuu kama wakristu.

Uhusiano wetu na Kristu umejengwa katika msingi wa upendo, hivyo ndivyo anavyotuambia Yohane katika somo la pili. Mungu ni upendo, kwa upendo wake ametuumba, ametukomboa, anaendelea kututegemeza na atatupa tuzo ya urithi wa mbingu milele. Kila tunapopendana tunakaa ndani ya Mungu, tunamualika Mungu kati yetu na Mungu anakaa ndani yetu. Upendo wa Mungu unajidhihirisha katika unyenyekevu. Ni rahisi sana mtu kuonesha unyenyekevu kwa mtu aliye mkubwa wake, kiumri ama kicheo au yule aliye na vipaji vingi kumzidi. Hebu fikiri ilivyo ngumu kwa mtu kujinyenyekesha kwa mdogo wake kiumri ama kicheo au kwa mtu aliyemzidi katika elimu ama vipaji na karama mbalimbali. Hivi ndivyo Mungu alivyotupenda, yeye aliyekuwa Mungu akatwaa hali ya utumwa ili atutumikie sisi viumbe vyake


Ikiwa kila mkristu ataona kuwa maisha ya hapa duniani ni maandalizi tu ya maisha mazuri na yenye raha mbinguni, itakuwa ni motisha tosha ya kupambana siku hadi siku  ili kufikia maisha hayo. Tuombe kwa Mungu ili daima tutafute kuwa mashuhuda wake kwa maneno na matendo yetu ili kufikia ukamilifu anaoutegemea kwetu.

1 comment:

  1. Online blackjack table game - Ozlemgultekin
    Online blackjack table game - 4 player online blackjack. Free spins - bonus round; 바카라 사이트 쿠폰 Free spins - 안전 바카라 사이트 bonus round; Free spins - bonus round; Free spins - bonus round; Free spins - bonus 실시간 바카라 사이트 round; 넥스트 바카라 Free spins - bonus round; Free spins - bonus round; Free spins - bonus round; Free 온라인 바카라 사이트 spins - bonus round; Free spins - bonus round; Free spins - bonus round;

    ReplyDelete