I.
Mdo
9:26-31, II. IYoh 3:18-24, Inj. Yn 15:1-8
Sisi tumefanywa kuwa
watoto wa Mungu kwa ukombozi wa Kristu. Tumewekwa huru dhidi ya utumwa wa
dhambi na hakika huu ndio uhuru wa kweli. Hatuwezi kuendelea kuwa wana wa Mungu,
kuwa na uhuru huu wa kweli ikiwa tutatetereka katika imani, imani inayodai
kujiunganisha maisha yetu na Kristu. Masomo ya leo yanatuelekeza katika kuishi
fadhila zitakazoimarisha uhusiano wetu na Kristu
Yesu ni mzabibu wa
kweli maana yake Yesu ndiye wokovu wetu wa kweli. Tawi lisilokaa ndani ya
mzabibu haliwezi kuzaa na mkulima huliondoa, lakini lile likaalo ndani ya mzabibu
huzaa na mkulima hulisafisha vizuri ili lizae sana. Sisi tu matawi ya Yesu
aliye mzabibu wa kweli. Kama tukichagua kukaa ndani ya Yesu tutazaa matunda, la
tusipokaa ndani yake tutanyauka, tutaondolewa na kutupwa motoni na kuteketea. Yeyote
anayekaa ndani ya Yesu, Yesu hukaa ndani yake pia naye huzaa sana. Mkristu
anayekataa kusikia sauti ya Yesu na kuenenda kadiri ya maelekezo ya ulimwengu
atanyauka na kuteketea kiroho na kimwili jehanum. Pia yule mkristu anayemkiri Yesu
kwa mdomo tu lakini kimatendo yuko mbali naye atanyauka na kuteketea jehanum. Wale
ambao wanamfuata Yesu wakati wa raha tu lakini wanapopata misukosuko
wanamkimbia watanyauka pia. Bila Kristu hatuwezi kitu. Mkristu atakuwa ndani ya
Kristu daima kwa kusali mara kwa mara, kusoma na kutafakari neno la Mungu na kwa
namna hii atamtukuza Mungu daima.
Mtume Yohane katika
somo la pili anatufundisha kwamba kuwa mkristu maana yake ni kuwa na imani
sahihi katika Kristu na kutenda au
kuishi kadiri ya imani hiyo sahihi. Imani yetu inapaswa kuwa katika jina la
Yesu, yaani nafsi ya pili ya Mungu aliyefanyika mwili akakaa kwetu, akaishi
sawa nasi katika kila kitu lakini hakutenda dhambi. Alikufa kwa ajili yetu na
akafufuka katika wafu li kutupa tumaini jipya na alikwenda kutuandalia makao ya
milele mbinguni. Yesu huyu alitupa amri ya mapendo akatutaka tumuige yeye kama
tunataka kufikia utukufu. Mtume Yohane anarudia wazo la Kristu katika injili kuwa yeyote anayezishika
amri zake kwa maneno na matendo yake huyo anakaaa ndani yake na Kristu anakaa
ndani ya mtu huyo. Mtume Yohane anasema tukiishi namna hii tutakuwa na amani ya
roho kwani dhamiri zetu hazitatusuta. Yeyote anayeishi kwa ujanjaujanja, uwongo
na unafiki moyo wake daima humsuta na kumhukumu na hawezi kuwa na uhuru na
amani ya Mungu
Katika somo la kwanza Paulo
baada ya kuongoka alianza kuhubiri habari ya Kristu mfufuko yule aliyekuwa
anamtesa kupitia wafuasi wake. Kwa sababu
ya historia yake mbaya dhidi ya wakristu, waamini wa Yerusalem wanasita
kumpokea anapojaribu kujiunga nao. Ni jambo la kawaida pengine kwa hicho
walichokifanya wakristu hao, hata mimi na wewe leo hii tungeweza kuwa na wasiwsi
kama wao. Wakati wakristu wengine wanahisi kuwa Paulo anakuja kuwapeleleza
Barnaba anafanya kitu cha kijasiri cha kutanguliza mtazamo chanya kwa Paulo ili
kumpa nafasi ya kuthibitisha uzuri wake.Barnaba pia anatufundisha kuwa tusiwahukumu
watu kwa maisha yao ya zamani bali kwa jinsi wanavyoishi sasa. Walau tuamini
kuwa kuna uwezekano wa wadhambi kuongoka kama ambavyo inaweza kututokea sisi
katika maisha yetu. Wapo watu ambao wakishamchukulia mtu kuwa mbaya hiyo
itadumu daima bila kuruhusu uwezekano wa kubadilika, hii ni mbaya kwa mkristu. Hivyo
pamoja na tahadhari tunazochukua lakini tuweke uwezekano wa wema pia. Huu ndio
upendo wa Kristu.
Si jambo rahisi kuishi
fadhila hizo tulizoziona katika masomo ya leo. Utakatifu wa maisha unafikiwa
kwa kufanya sadaka kubwa. Tunapaswa kupigana vita kubwa ya Kiroho na kuishinda.
Ni ajabu kuwa pamoja na kufahamu ukweli
huu na ya kwamba tunahitaji msaada wa
Mungu katika jitihada zetu lakini tumekuwa wazito wa kutafuta msaada huo kwa
njia ya sala na mafungo. Kijana yupo tayari kusali novena na kufunga chakula
kwa siku kadhaa kwa ajili ya kuomba mchumba mwema, kufaulu mtihani au kupata
kazi kitu ambacho ni kizuri, lakini hawezi kufanya hivyo kwa ajili kuomba neema
ya kumsaidia asifanye tendo la ndoa kabla ya ndoa na mchumba wake. Daima atabaki
na kusema tuu, aah ni udhaifu tu wa kibinadamu au ni shetani tu. Hakika tunahitaji
kusali sana na kufunga ili tubaki tumeunganika Kristu daima.