Thursday, 2 April 2015

IJUMAA KUU YA MATESO YA BWANA. APRIL 3, 2015

Somo I. Isa 52:13-53:12, Somo II. Ebr 4:14-16; 5:7-9, Injili. Yn 18:1-19:42
Kanisa zima linaadhimisha leo mateso na kifo cha Bwana wetu Yesu Kristu msalabani. Ni siku ya kwanza katika siku kuu tatu za pasaka ambayo tumeianza jana kwa adhimisho la karamu ya mwisho. Leo historia ya mateso ya Bwana wetu Yesu Kristu inasomwa kadiri ya mwinjili Yohane. Tafakari yetu leo itatazama ushiriki wa wahusika  mbalimbali katika historia hiyo ili wahusika hawa wawe kama kioo cha kujitazamia uhusiano wetu na Kristu pamoja na wenzetu pia.

Mtume Petro ni mhusika anayemuendea Yesu katika ukweli na wala hakuwa na unafiki. Petro alimpenda sana Yesu na daima aliishi kama alivyo, alinena na kutenda kile alichoamini kuwa kinafaa machoni  kwa Yesu, pale alipotenda mazuri Yesu alimpongeza na pale alipotenda mabaya Yesu alimkemea ili ajirudi. Maisha ya Petro yamekuwa ni ya kuanguka na kuinuka.  Maaskari wanapokuja kumkamata Yesu, Petro anamkata sikio mmojawapo wa wale waliokuja kumkamata kwa upanga. Yesu anamsihi Petro arudishe upanga wake ili mpango wa Mungu utimie. Baada ya Yesu kukamatwa wanafunzi wengine wanakimbia lakini Petro anamfuata Yesu mpaka ndani mbele ya Kuhani mkuu. Baadae Petro aliyeonesha ushujaa mkubwa katika kumpigania Bwana wake aliyempenda anaanguka kwa kumkana mara tatu. Ni kweli Petro ameanguka lakini ameanguka katika mazingira ya kumfuata Yesu Kristu na ndio maana alipogundua amekosa aliamka tena kwa kutubu. Yesu anamsamehe Petro na kumuweka kuwa kiongozi wa kwanza wa kanisa lake kwa sababu moyo wa Petro daima ulimtafuta Yesu, umeanguka katika safari ya kumtafuta Yesu, Petro ameamka ili aendelee mbele.

Annas ni mhusika fisadi aliyedhamiria kumuangamiza Yesu hata ikibidi kwa kukiuka misingi ya haki kwasababu alimpinga katika ufisadi wake. Annas alikuwa ni mmiliki vibanda au maduka yaliyokuwa yanauza wanyama na vitu mbalimbali kwa ajili ya kutolea sadaka hekaluni  na biashara hiii ilifanyika ndani ya hekalu. Wauzaji wa vitu hivi kwa ajili ya kutolea sadaka waliwauzia watu kwa bei kubwa sana kuliko kama wangenunua nje ya hekalu kiasi kwamba maskini walishindwa kumtolea Mungu wao sadaka. Watu walilazimika kununua vitu hivi ndani ya hekalu kwa sababu vitu vilivyonunuliwa nje daima vilichunguzwa ubora wake kama vinafaa na mara nyingi kama si mara zote vilikataliwa. Hivyo Annas aliye wahi kuwa kuhani mkuu huko nyuma, kati ya mwaka 6 B.K n 15 B.K , alijipatia faida hekaluni kwa kuwanyonya maskini. Kadiri ya mwinjili Yohane,( Yn 2:15-25), Yesu alikasirishwa sana na vitendo hivi vilivyonajisi hekalu na kuamua kuwatimua wafanya biashara hekaluni. Annas,  akiwa bado ana ushawishi katika ofisi ya kuhani mkuu ambayo kwa wakati huu ilikuwa inakaliwa na shemeji yake Kayafa na pia kwa watawala, anaamuru Yesu aletwe kwake kwanza kabla ya kwenda kwa Pilato. Wayahudi walikuwa na sheria kuwa mtu hawezi kuhukumiwa kwa ushahidi wake mwenyewe hivyo hapaswi kuulizwa maswali ili atoe ushuhuda wake mwenyewe, lakini Annas anakiuka misingi hiyo kwa kumuuliza Yesu swali na Yesu anamkumbusha juu ya utaratibu kwamba awaulize watu , wao ndio watatoa ushuhuda juu yake. Yesu akahukumiwa kabla ya kesi kusikilizwa maana watu hawakuulizwa watoe ushuhuda.

Wayahudi ni wahusika wenye chuki kubwa sana dhidi ya Yesu kiasi kwamba inawaziba, macho, akili na mioyo yao wasione, wasiwaze wala kuamua sawaswa. Wayahudi tangu mwanzo walipinga vikali kulipa kodi kwa Kaisari na sababu yao kubwa ilikuwa kaisari ni mpagani, Mungu pekee aliye mfalme wao ndiye anastahili kupokea kodi yao. Mafasarisayo wanapomwendea Yesu na kumuuliza juuu ya uhalali wa kulipa kodi kwa kaisari(Lk 20:22), wanataka kumtega kuona kama na yeye anawaunga mkono ama la ili kupima Umasiya wake. Pia wayahudi tangu mwanzo walijitambua kama taifa linalooongozwa na mfalme mmoja tu naye ni Mungu (1Sam 12:12), lakini leo Pilato anapowauliza nimsulibishe mfalme wenu wanajbu kwa nguvu kabisa kuwa wao hawana mflame isipokuwa kaisari yule ambaye wanakataa kumpa kodi kwa sababu ni mpagani,  yule ambaye hawamtambui. Hii yote ni kwa sababu ya chuki.

Pilato ni mhusika asiyekuwa jasiri katika kusimamia mambo ya msingi na hasa haki. Pilato tayari alishaingia katika mgogoro na wayahudi, na wayahudi walimshitaki kwa Kaisari. Linapotokea hili Pilato anaogopa asipofuata matakwa yao watampeleka tena kwa kaisari na kibarua chake kitakua matatani kwasababu tayaria ana onyo. Pilato anafanya kituko kingine anapoweka chapa juu ya msalaba wa Yesu iliyokuwa inasema Yesu Mnazareti Mflame wa Wayahudi, Wayahudi walipombishia asiandike hivyo alishupalia msimamo wake, akasema niliyoandika nimeyaandika. Pale ambapo alitakiwa awe na msimamao katika kuhakikisha jambo la msingi kama haki ya kuishi inalindwa ameshindwa kushupalia msimamo wake hali aikijua fika kuwa Yesu hana kosa, lakini kwenye hili la chapa ambalo halina madahara yeyote haogopi macho ya Wayahudi anasimamia msimamo wake. Hata kwenye maisha yetu tunaweka msimamo kwenye mambo yasiyo na msingi lakini kwenye mambo muhimu hatuwi na msimamo thabiti.

Maaaskari waliokuwa chini ya msalaba ni wahusika wasiojali mahangaiko ya watu bali maslahi yao kwanza. Walikuwa wanahangaika kugawana vazi la Yesu kwa kulipigia kura liwe la nani. Yesu anateseka sana msalabani lakini wao si kitu kwao, lililo  muhimu ni mali zake wazigawane vipi . Ni mara ngapi tumewashuhudia watu wakikimbilia mifukoni mwa majeruhi wa ajali kutafuta pesa, simu na vitu vingine vya thamani na kuwaacha wakihangaika hadi kufa. Lori la mafuta limepata ajali watu wanakimbilia kuchota mafuta badala ya kuokoa majeruhi. Ndugu katika familia wanaanza kugombania mali za baba wa famiila anayekaribia kukata roho kitandani. Tumepoteza roho ya huruma na kuwajali watu katika mahangaiko yao. Wakati mwingine si lazima tuchukue mali zao, lakini tuko tunahangaika ili tupige picha tuzitume kwenye mitandao ya kijamii. Hatuna moyo wa huruma na kuwasaidia watu katika mahangaiko yao.

Kila mmoja akiingia ndani ya moyo wake leo anapomuona Yesu anateseka anajivika uhusika upi kati ya hao wanaojitokeza katika simulizi la mateso?. Tukumbuke basi siku ya leo ni ya kujiweka chini ya Yesu wa msalaba na kumuomba msamaha pale tuliposhiriki katika kumsulibisha na pia kuzidi kumuomba neema yake atuimarishe pale tuliposhiriki katika kumpigania na kumtetea ili tuzidi kumpenda daima.


No comments:

Post a Comment