Monday, 13 April 2015

DOMINIKA YA TATU YA PASAKA, MWAKA B. APRIL 19, 2015

Somo I. Mdo 3:13-15, 17-19a, Somo II. 1Yn 2:1-5a, Injili. Lk 24:35-48
      
Kristu mfufuka analeta habari njema ya ondoleo la dhambi. Neno la Mungu laendelea kutusisitiza kuwa ufufuko wa Kristu ni ushindi dhidi ya dhambi na hivi namna sahihi ya kuupokea na kuuishi ufufuko huo ni kutafuta nafasi ya mara kwa mara ya kujipatanisha na Mungu wetu kila tunapoanguka dhambini na hasa dhambi za mauti.

Katika injili leo Kristu anawatokea mitume katika chumba na akiwa huko anakula chakula pamoja nao baada ya kuwaonesha makovu ya mikono yake na miguu yake. Yesu anayafanya haya ili kuthibitisha kuwa katika ufufuko wake yeye si  roho tupu wala si mzuka bali ni Mungu kweli na mtu kweli ambaye mwili wake wa kibinadamu  haukuhairibiwa wala kupotea katika kifo bali umegeuzwa na kuwa katika hali ya utukufu. Kwa kuonesha makovu ya miguu na mikono yake Kristu analenga pia kuonesha kuwa ufufuko wake umekuja baada ya kuvumilia mateso makali ya msalaba kwa ajili ya wokovu wetu. Hivi ndivyo tutakavyokuwa siku ya mwisho atakakapokuja. Sisi sote tunatumwa kuwahubiria watu kuwa sasa tumepata ondoleo la dhambi kwa ufufuko wa Kristu.

Petro katika somo la kwanza anawatangazia watu habari ya toba. Anawaeleza Wayahudi kuwa, pamoja na kwamba walimkana Yesu mbele ya Pilato aliyetaka kumfungulia Yesu lakini wao wakataka mhalifu ndiye afunguliwe yaani Baraba lakini Yesu asiye na hatia ndiye auawe, Kristu mfufuka anawasamehe dhambi yao kwa kuwa hawakujua watendalo. Anawaalika watubu warejee ili dhambi yao ifutwe kwasababu sasa wamejua maana ya mambo yote yaliyotokea kama yalivyoaguliwa na manabii tangu zamani. Wayahudi hawakujua watendalo lakini sasa wamejua ni heri kwao lakini wanawajibika sasa kuishi toba vinginevyo adhabu inawangoja. Yeyote anayeshupaa katika ouvu hata baada ya kuoneshwa uovu wake na kuonywa ataangamia.

Katika somo la pili mtume Yohane kawenye barua yake anawaasa wakristu wote juu ya kuepuka dhambi  na daima wawe wepesi wa kuungama pale wanapoanguka. Yohane amekwishatueleza kwenye sura ya kwanza ya barua hii kwamba ni uongo kwa mtu kusema hana dhambi na kweli haimo ndani yake. Mtume Yohane anaona hatari kubwa ya watu kubweteka kutokana na maeno haya wasione haja tena wala wasipate  msukumo wa kujibidiisha katika kuepa dhambi. Yohane pia kwenye sura hiyo ya kwanza anasisitiza kuwa tukiziungama dhambi zetu yeye (Kristu) ni mwaminifu atatusamehe dhambi. Kuna hatari pia watu wakaitumia vibaya huruma hii na wasione haja ya kuungama wakiamini kuwa huruma itakuja tu. Katika somo la leo Yohane anaweka msisitizo juu ya kuepuka dhambi na umuhimu wa kuziungama dhambi zetu. Kumjua Mungu maana yake ni kushika amri zake.


Kuepa dhambi ni vita kubwa sana kwani shetani hapendi kabisa kuona kuwa tunaongoka. Vita hii inahitaji utayari wetu, ujasiri na jitihada zetu tukipata nguvu kutoka kwa Mungu mwenyewe. Lazima tutambue kuwa hakuna njia nyingine zaidi ya kujipatanisha na Mungu wetu ikiwa tunataka kufurahia matunda ya utukufu wa ufufuko.

No comments:

Post a Comment