Wednesday, 22 April 2015

DOMINIKA YA NNE YA PASAKA, MWAKA B. APRIL 26, 2015

Somo I. Mdo 4:8-12, Somo II. 1Yn. 3:1-2, Injili Yn 10:11-18
Tunapoendelea kufurahia ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristu leo tunaalikwa kujitahidi kadiri inavyowezekana kwa kutegemea msaada wake Mwenyezi kubaki katika kundi la kondoo wa Kristu yaani kanisa lake. Yeye Kristu ni mchungaji mwema, daima anatupigania na kutulinda dhidi ya mbwamwitu wakali. Iwapo tutatoka katika kundi, na kutangatanga nje ya kundi, tutajiweka katika hatari ya kushambuliwa na mbwa mwitu wakali, lakini pia tunaweza kujikuta tumeangukia mikononi mwa wachungaji wanaofanya kazi kwa mshahara na hivyo kutojali sana usalama wetu.

Katika injili Yesu anasema kuwa yeye ni mchungaji mwema na kweli ndivyo alivyo. Ni mchumgaji mwema wa kondooo wake ambao ndio sisi wakristu. Ni mchungaji mwema kwa sababu yuko tayari kutoa uhai wake ili kutuokoa kutoka katika mikono ya mwbwa mwitu shetani anayetafuta kutumaliza. Anafanya kazi yake si kwa sababu anatafuta faida yake binafsi bali kutokana na upendo alionao. Anajua wazi kuwa kupoteza uhai wa kimwili kwa ajili ya kutulinda sisi si kitu kwake kwani ni njia ya kufikia utukufu, atausalimisha uhai huo katika ufufuko katika hali ya utukufu. Ni mchungaji mwema kwasababu anawajua kondoo wake na yuko tayari kuwatafuta kondoo wote waliopotea na kuwarudisha kundini.

Wakristu tulio kondoo wa Kristu tunatumwa kufanya kazi kati ya mbwa mwitu wakali, shetani na wafuasi wake wanaopinga kazi ya Kristu. Tuko katika hatari kubwa ya kiroho na kimwili. Shetani daima anatafuta nafasi ya kuangamiza uzima mpya tulioupokea katika ubatizo na katika sakramenti zingine hasa ekaristi na kitubio. Uzima unaotusadia kuepuka dhambi na kuendelea kumtumikia Mungu daima. Shetani pia anatafuta nafasi ya kuondoa uhai wetu wa kimwili ili kutoa vitisho kwa kondoo wengine ili watawanyike na  kumuacha nyuma mchungaji wao ha hivyo iwe rahisi kwake kuwakamata na kuwaangamiza. Neno la Mungu leo linalenga kutuondolea hofu dhidi ya Mbwa mwitu shetani. Tunaye mchungaji mwema ambaye yuko tayari kutoa uhai wake ili kulinda na kutetea uhai wetu wa kiroho tulioupokea kwa sakramenti. Lakini yupo tayari pia kutuondolea hofu dhidi ya kifo tunapofanya kazi ya kumtangaza. Kifo cha mwili si kitu kwetu ikiwa tuna uzima wa kiroho kwani ni mlango wa kufikia ukamilifu wa uzima huo wa kiroho mbinguni.

Katika somo la pili mtume Yohane anatueleza juu ya bahati tuliyo nayo ya kuwa wana wa Mungu. Kwa Kristu mchungaji mwema kuutoa uhai wake ametukumboa kutoka katika mikono ya shetani na kutufanya si watoto wa shetani tena bali wana wa Mungu. Uhusiano wetu umekuwa si tu wa Muumba na viumbe vyake bali Baba na wana wake. Ni uhusiano wa ndani uliojengwa katika misingi ya upendo. Mungu aliye Baba yetu yuko tayari kutupigania na kututetea dhidi ya muovu shetani ambaye kama alivyomuandama Kristu ataendelea kutuandama pia.  Tunafanywa kuwa wana wa Mungu kwa neema yake Baba kwetu lakini pia kwa jinsi tunavyopokea neema hiyo. Hakuna anayeweza kuwa mwana wa Mungu kama hajapokea mwaliko wa kuwa mwana kwa kuishi maisha ya nuru. hawa ndio kondoo ambabo Kristu asema kuwa walio wake anawajua nao wanamjua. Kufanyika wana wa Mungu ni mwanzo wa safari ya kuelekea kufanana na Mungu pale tutakapomuona uso kwa uso siku ya mwisho Kristu atakapokuja.

Katika somo la kwanza mitume wakiongozwa na Petro wanapata ujasiri wa kuendelea kumhubiri Kristu mfufuka mbali ya kupokea vitisho vya kuuawa kutoka kwa wakubwa wa watu na wazee wa Israeli. Ujasiri huu unatokana na Imani yao kwa kristu aliyekwisha kuambia tayari kuwa yeye ni mchungaji mwema yuko tayari kuwapigania kondoo wake dhidi ya mwovu shetani anayepambana kuwanyima watu mbingu. Ufufuko wa kristu umewathibitishia ukweli huo sasa hawana hofu tana na kifo ambacho shetani hutumia ili kuwakatisha tamaa wana wa Mungu katika jitihada zao za kumhubiri Kristu.

Kristu mfufuka anatupigania daima katika maisha yetu. Pamoja na kwamba Kristu anatulinda dhidi ya hatari za kimwili pia, lakini hasa yuko tayari kutoa uhai wake ili tusipoteze uhai wa Ki-Mungu ndani ya roho zetu  yaani neema ya utakaso tunayoipata kwa kupokea sakramenti zake. Anapotulinda uhai wa kimwili anataka bado tuendelee kuishi duniani ili tuufanyie kazi uhai wa Ki-Mungu  ndani ya roho zetu. Vinginevyo magonjwa, mateso, mahangaiko na hata vifo vinavyotokea kwa wana wa Mungu havina madhara kwa uzima wa Ki-Mungu ndani ya roho zetu  ila badala yake vikipokelewa kwa imani ni njia ya kupata  uzima wa milele Mbinguni.


No comments:

Post a Comment