Saturday, 4 April 2015

DOMINIKA YA PASAKA, MWAKA B. APRIL 5, 2015

Somo I. Mdo 10:34, 37-43, Somo II.  IKor. 5:6-8, Injili. Mk 16:1-7

Leo kanisa linaadhimisha fumbo la ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristu.  Masomo ya leo yaeleza kuwa ufufuko wa Kristu ni ushindi na  ya kwamba sisi tunatumwa kuwa mashahidi wa ushindi huo kwa maneno na matendo yetu. Ufufuko wa Kristu unaleta maisha mapya, maisha katika Kristu, maisha ya milele  ambayo mwanzo wake ni hapa duniani na ukamilifu wake ni mbinguni. Wale wanawake watatu waliokwenda kaburini kadiri ya injili ya leo walikuta kaburi li wazi na tupu, halina mwili. Lakini pale ulipolazwa mwili waliona vitambaa alivyofungwa Yesu vimelala. Yesu amefufuka maana yake uzima wake wa kibinadamu wa kimwili kupitia kifo chake umegeuzwa na kuwa uzima mpya wa umilele, uzima usiokuwa na mipaka ya muda na mahali  uzima usiokuwa na mahangaiko tena na ndio maana sanda na vitambaa vingine  alivyofungwa wakati wa kuzikwa vilibaki kaburini Yesu alipofufuka. Hivyo ufufuko wa Yesu maana yake ni kupata maisha mapya ya umilele katika mwili mpya wa utukufu. Sisi sote baada ya kumaliza maisha ya hapa duniani tukiwa wenye imani tutafufuliwa na kuwa kama Yesu na kuingia kwenye furaha ya milele na miili yetu ya utukufu.

Petro anahubiri juu ya Kristu mfufuka katika somo la kwanza. Petro anatoa ushuhuda kuwa ufufuko ni ushindi dhidi ya mateso na kifo cha mwili. Wayahudi walimwua lakini Mungu alimfufua siku ya tatu. Si tu ushindi dhidi ya kifo cha mwili lakini Petro anasema kuwa ufufuko huu ni ushindi dhidi ya kifo cha roho yaani dhambi na ndio maana anamalizi kwa kusema kuwa kila amwaminiye atapokea ondoleo la dhambi, maneno yale ambayo Kristu alimwambia Martha kuwa kila amwaminie ajapokufa atakuwa anaishi(Yn 11:25). Petro anasema kuwa Kristu aliwaamuru wawe mashuhuda wa habari hii njema ya ufufuko kwa maneno na maisha yao. Lazima kila mkristu aushuhudie ufufuko wa Kristu kwa kuhubiri na kuishi vema. Unapozidi kushupaa katika dhambi bila kutafuta nafasi ya kufufuliwa na Kristu wewe huamini  kwamba Kristu alifufuka.

Katika somo la pili mtume Paulo anatuasa kuwa maisha ya ufufuko yanadai kuachana na chachu ya kale yaani dhambi na kuwa donge jipya yaani mioyo mipya. Sisi  tuliofufuka pamoja na Kristu hatupaswi tena kuridhika na dhambi. Paulo anaongea haya katika mazingira ambapo katika kanisa la Korintho kulikuwa na maovu makubwa, uasherati ulizidi kiasi cha mtu kutembea au kulala na mke wa baba yake yaani mama yake wa kambo. Kilichomkasirisha Paulo ni kwamba kama jumuiya ya waamini walilifumbia macho jambo hili, wakaridhika na maisha yaliendelea kama kawaida. Paulo anawaambia wasikubali kuwa karibu na dhambi wakaridhika kwani dhambi ni kama chachu ambayo inasambaa taratibu mpaka ngano yote inachachuka. Watu taratibu wataanza kuiga mfano baya wa mtu huyu wakiona kuwa ni kawaida. Tunapaswa tushtuke, tusikitike tuone uchungu kila tunapoona matendo maovu yakifanywa na watu wengine au na sisi na tuchukue hatua. Tuna uhakika kwamba mapamabano yetu dhidi ya dambi yatafanikiwa kwasababu tunaye Kristu aliyeshinda dhambi kwa ufufuko wake.

Katika somo la injili, mwinjili Marko anatueleza habari ya ufufuko wa Kristu. Marko pekee kati ya wainjili wote anasimulia kuwa yule mjumbe wa Mungu aliyewaambia wale wanawake habari ya ufufuko alitamka kwao kuwa waende  wekawaambia wafuasi na Petro kwamba Kirstu mfufuka amewatangulia Galilaya.   Marko anaweka msisitizo si tu kwamba wakawaambie wafuasi lakini na Petro. Kwa maneno haya Marko anataka kuonesha kuwa ufufuko wa Yesu umeshinda dhambi ya Petro ya kumkana Bwana wake mara tatu. Petro kwa sababu alimwamini na kumpenda Yesu hata alipokufa katika dhambi ya kumkana Yesu anaendelea kuishi. Petro anaishi kwa sababu hakuridhika na kumkana Yesu, tendo lile lilimpa uchungu, masikitiko na mahangaiko ya moyo na hivyo akatafuta nafasi ya kuamka na kuanza tena na kwa sababu hiyo Kristo alimfufua.

Ufufuko wa Kristu unapaswa kutupatia mtazamo mpya wa maisha yetu ya hapa duniani. Tunapaswa sasa kuyaona maisha ya hapa duniani kama maandalizi ya maisha ya milele. Tukiyatazama mambo yote ya ulimwengu huu kama msaada wa kutufikisha kwa Mungu hatutakuwa na hofu tena, hofu ya mambo ambayo dunia inayaona kuwa ndio kila kitu. Hatutakuwa na hofu ya kifo tena kwasababu ni mlango wa maisha ya umilele. Tutakuwa watu wa kutoa zaidi kuliko kupokea, watu wa kutumikia zaidi kuliko kutumikie. Hatuna hofu ya kupoteza wala kuwa masikini kwa kutoa, hofu ya kudhalilishwa kwa kutumikia, hofu ya kuchekwa kwa kutunza ubikira mpka siku ya ndoa takatifu.


No comments:

Post a Comment