Wednesday, 1 April 2015

ALHAMISI KUU. April 2, 2015

MISA YA KARAMU YA BWANA
Somo I. Kut 12:1-8, 11-14,  Somo la II. I Kor 11:23-26, Injili. Yn 13:1-15

Adhimisho la Karamu ya Bwana ndio mwanzo wa siku tatu kuu za pasaka yaani Ijumaa kuu, Jumamosi Kuu na Dominika ya Pasaka siku ambazo kanisa linatafakari mateso, kifo na ufufuko wa Bwana. Hivyo siku tatu kuu za pasaka zinaanza kwa adhimisho hili na kuishia na masifu ya jioni ya pili ya Dominika ya pasaka. Leo kanisa kwa adhimisho hili la karamu ya Bwana linakumbuka mambo matatu; Kuwekwa kwa Sakramenti ya Ekaristi takatifu, Kuwekwa kwa Sakramenti ya Daraja na Amri kuu ya Upendo kwa Jirani.

Yesu alikuja duniani ili tuwe na uzima na ameanza tayari kazi yake hiyo katika maisha yake ya hapa duniani na kwa namna ya pekee kwa kifo chake pale msalabani. Baada ya ufufuko Yesu anapaa mbinguni lakini anataka aendelee kutupatia uzima kama alivyokuwa anafanya hapa duniani hadi ukamilifu wa dahari. Ili kufanikisha hilo anaweka ekaristi yaani mwili na damu yake. Katika ekaristi takatifu Yesu anaendelea kubaki nasi ili  kutupa uzima pamoja na kwamba alisharudi kwa Baba. Kwa maneno haya “twaeni mle wote huu ndio mwili wangu utakaotolewa kwa ajili yenu” na “twaeni mnywe wote hiki ni kikombe cha damu yangu, damu ya agano jipya la milele, itakayomwagika kwa ajili yenu na kwa ajili ya wengi kwa maondoleo ya dhambi, fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu”, Yesu anaweka sakramenti ya ekaristi. Tuipokee sakramenti ya ekaristi kwa uchaji ili tupate uzima wa milele

Yesu alikuja Duniani ili kuanzisha safari ya ukombozi. Alifanya kazi hii kwa kufundisha, kuponya magonjwa, kulisha watu chakula cha mwili na roho, kuwapa faraja watu na kilele chake ni kifo cha msalaba. Baada ya ufufuko Yesu anarudi kwa Baba yake lakini anataka habari hii njema ya ukombozi wake iwafikie vizazi vyote hadi ukamilifu wa dahari. Anaweka sakramenti ya daraja ili kuwepo watu watakaomwakilisha na kufanya kwa niaba yake hapa duniani. Mitume wanawekwa rasmi kwa kazi hiyo kwa maneno haya “fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu”, nao wanawarithisha vizazi vya mbele yao kazi hiyo kwa kuwawekea mikono.

Yesu katika karamu ya mwisho anaweka amri mpya ya mapendo kwa Mungu na kwa jirani. Mapendo yanayodai kujinyenyekesha kwa hali ya juu kwa ajili ya kuwahudumia wengine. Tunajifunza yafuatayo kuhusu kuwekwa kwa amri ya mapendo kadiri ya injili ya leo;

Yesu hali akijua kuwa amepewa mamlaka yote na Baba yake na kwamba saa yake ya kutukuzwa imefika,  hadhi ii kubwa haikumpa kiburi na badala yake alijinyenyekesha kiasi cha kuwaosha miguu mitume wake kazi iliyofanywa na watumwa. Unapogundua kuwa una karama fulani au cheo fulani unapata kiburi na kujiona mtu wa kutumikiwa zaidi au unajinyenyekesha na kutumikia?

Yesu alijua kuwa ametoka kwa Mungu na ya kwamba anarudi kwake lakini hali hii haikumfanya awadharau wanadamu na kuwa mbali nao kana kwamba sio wa aina yake badala yake ndio wakati hasa  alikuwa karibu nao  kiasi cha kufanya kazi ya watumwa ya kuwaosha wengine miguu. Kadiri unapokuwa karibu zaidi na Mungu kwa matendo yako mema unajiona kuwa hupaswi kuongea na kuwakaribia wadhambi au unatafuta nafasi ya kuwaonesha upendo wa Mungu ili wamuongokee?

Yesu  pia alijua kuwa saa yake ya kusalitiwa na kukanwa na Yuda na Petro, kwa namna ya pekee, imefika. Hili halikumfanya Yesu awake hasira na chuki dhidi ya mitume wake na hasa Yuda na Petro. Badala yake Yesu anawaka moto wa mapendo kwao kiasi cha kuwaosha miguu kama mtumwa afanyavyo kwa bwana wake.


Adhimisho la Karamu ya Bwana litusidie ili tumpokee Yesu wa ekaristi kwa imani na uchaji, tuwapokee mapadre kama Kristu mwingine, na tujibidiishe katika kuishi upendo katika kweli.

2 comments:

  1. Great homily padre keep up as days go on the blog will improve and become informative on pastoral issues even through photos

    ReplyDelete
  2. Tumshukuru Mungu Bwana James

    ReplyDelete